Hatua zaidi zinahitajika kukabiliana na usafirishaji haramu!

Play all audios:

Kwamujibu wa ripoti ya takwimu za kimataifa kuhusu usafirishaji haramu wa watu iliyozinduliwa tarehe 7 Januari 2019 mjini Vienna, Austria inasema kuwa idadi ya waathirika wa usafirishaji
haramu imeongezeka, huku idadi ya makundi yaliyojihami na magaidi wanawasafirisha wanawake na watoto kwa ajili ya kupata fedha na kuwaandikisha kama wafuasi.
Mkurugenzi mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kupambamba na madawa ya kulevya na uhalifu, UNODC, Yury Fedeotov akiwasilisha ripoti hiyo ambayo imetathmini nchi 142 kuhusu mienendo ya
usafirishaji haramu na uhalifu huo katika maeneo ya mizozo ya silaha, amesema, “watoto wanaotumikishwa jeshini, kazi ya lazima utumikishwaji kingono, usafirishwaji haramu umechukua sura mpya
ya kusikitisha wakati vikundi vilivyojihami na magaidi wakisambaza hofu na kutumia vishawishi ili kuwapata wafuasi wapya.” Bwana Fedotov amesema ripoti imeonesha wazi kuwa kuna haja ya
kuimarisha ufadhili wa kiufundi na ushrikiano, kusaidia nchi kulinda manusura wake na kuwawajibisha wahalifu mbele ya sheria ili kufikia malengo ya maendeleo endelevu, SDGs.
Akizungumza katika hafla hiyo maalum ya kamisheni ya kuzuia uhalifu na uhalifu wa kisheria wakati wa uzinduzi huo waziri wa maswala ya kigeni wa Austria,Bwana Karin Kneissl, ametaja umuhimu
wa ripoti kuangazia msaada kwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa katika kukabiliana na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu na utu. Kwa mujibu wa ripoti, kimataifa, nchi zinagundua na
kuripoti manusura wengi wa usafirishwaji haramu. Aidha ripoti imebaini kuwa kuna ongezeko la watoto wanaosafirishwa ikiwa ni asilimia 30 ya visa vyote na wakati huo wasichana wengi
wakiathirika zaidi ikilinganishwa na wavulana. Ukatili wa kingono ndiyo kichocheo kikubwa cha usafirishaji haramu, ikijumuisha asilimia 59 ya visa vyote.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa,wanathibitisha kuwa usafirishaji wa ndani upo kwa kiasi kikubwa kuliko ule wa kimataifa. Waathirika wakubwa wa biashara hii ni watoto hasa wasichana wadogo
wanaosafirishwa na kutumikishwa kwenye kazi za ndani na biashara ya ngono. Wahusika katika biashara hii hufanyishwa kazi kwa kulazimishwa ikiwamo kutumikishwa kwenye ngono tofauti na
makubaliano wakati wanachukuliwa. Huu ni utumwa wa kisasa ambao nchi yetu inapitia na bahati nzuri mamlaka husika wanakiri kwamba nchi yetu ina genge la watu wanaojihusisha nao. Hata hivyo
katika matataifa mengi pia wapo wazazi ambao bila kujua wanawashawishi watoto wao baada ya kurubuniwa na wasafirishaji kuwa huko waendako watafanya kazi kwa ujira mnono, lakini watoto
wanapofika hukutana na ukatili usio kifani.
Wachambuzi wa mambo wanasema watu walio hatarini kuingia kwenye biashara hii ni watu wasio na ajira, watoto yatima, wakimbizi na wale wanaotoka kwenye nchi zenye vita au machafuko. Kadhalika
katika nchi nyingine umaskini unatajwa kuwa moja ya sababu ya kuwepo kwa biashara haramu ya binadamu. Lakini inawezekana kabisa kupambana na biashara hii inayolenga kudhalilisha utu wa mtu
ili wengine wanufaike na jasho lao. Wapo watu wanaotumikishwa kwa kulipwa ujira mdogo kwenye mashamba ya matajiri, hotelini, madanguro na majumbani baada ya kutolewa vijijini kinyume na haki
za binadamu na sheria. Inawezekana kabisa kupambana na biashara hii ya utumwa wa kisasa ikiwa kila mtu anatahusika na kusimamia wajibu wake pale alipo.
Kwa usafirishaji wa ndani, wazazi na walezi wanapaswa kupewa elimu na kutoruhusu watoto wao kuchukuliwa kiholela na watu wasiowajua kwa ahadi mbalimbali. Kwa upande mwingine Serikali inaweza
kuzuia usafirishaji wa watu wake kwenda kufanya kazi nje bila kuthibitisha kupitia mikataba halali ya makubaliano ya kazi. kadhalika Idara za Uhamiaji zinapaswa kujiridhisha kutoka kwa
ubalozi wa nchi zao kwa watu hao wanaotaka kwenda kufanya kazi na kujua uhalali wa kampuni zinazowasafirisha. Kama biashara hii ya utumwa inaendelea kushamiri kwenye nchi zinazopambana ili
kufikia uchumi wa kati ni wazi kuwa mapambano hayo yatakuwa ni vigumu kufikia ukomo wake iwapo hakuna hatua za kuthibiti kwa dhati.